Monday, April 16, 2012

TOTO WAVUNJA UNDUGU NA YANGA - WAITANDIKA 3-2 . SIMBA YAIZIDI KUCHANUA

SIMBA SC wamejiimarisha kileleni mwa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania kufuatia ushindi wa 1-0 jioni hii kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, dhidi ya Ruvu Shooting.
Shukrani kwake kiungo wa kimataifa wa Rwanda, Patrick Mutesa Mafisango aliyefunga bao hilo pekee dakika ya 80.
Simba sasa ina pointi 53, tatu zaidi dhidi ya azam FC inayoshika nafasi ya pili.

CCM KIRUMBA MWANZA
Katika mchezo mwingine wa Ligi Kuu, kwenye Uwanja wa CCM Kirumba mjini Mwanza, wenyeji Toto African walifanya kile ambacho hakikutarajiwa na wengi.
Toto wamewafunga ‘baba zao’ Yanga mabao 3-2 kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza.
Mabao ya Toto inayopigana kuepuka kushuka daraja, yalitiwa kimiani na Mussa Said aliyefunga mawili dakika ya 18 na 39, Kulwa Mobbi dakika ya 24 Iddi.
Hamisi Kiiza aliifungia Yanga mabao mawili dakika ya 43 na 65.
Yanga inabaki na pointi zake 46 katika nafasi ya tatu, dhahiri sasa inaelekea kupoteza matumaini ya kutetea ubingwa wake wa Ligi Kuu.
Kocha Mserbia, Kosradin Papic alizomewa na mashabiki wa Yanga mjini Mwanza kutokana na kiwango kibovu ambacho timu hiyo inacheza hivi sasa.
Kipigo cha leo kinamaanisha Yanga imepoteza mechi mbili mfululizo, kwani mechi iliyopita na Coastal Union mjini Tanga, japokuwa walishinda 1-0, lakini walipokonywa pointi hizo na Kamati ya Ligi Kuu.

No comments:

Post a Comment