Thursday, August 14, 2014

Dola za Marekani milioni 53.8 zapatikana kutokana na mauzo ya vito

         

Tanzanite
 
 
Na Greyson Mwase, Bagamoyo
Jumla ya Dola za Marekani  milioni 53.8  zilipatikana kutokana na mauzo ya vito mbalimbali ndani ya nchi  kwa mwaka wa fedha 2013/2014.
Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Kitengo cha  Uchambuzi na Uthamini wa Madini ya Almasi na Vito, (TANSORT) kilichopo chini ya Wizara  ya Nishati na Madini   Archard Kalugendo kwenye semina  iliyoshirikisha Makamishna Wasaidizi wa Madini wa Kanda,  Afisa Madini Wakazi na  Wataalamu wa Wizara ya Nishati na Madini inayoendelea Bagamoyo  yenye lengo la  kujadili  utendaji na  uboreshaji wa  shughuli za uthaminishaji wa madini ya almasi na  vito nchini.
Kalugendo alisema kuwa  mauzo hayo  yanatokana na usimamizi mzuri wa Kitengo hicho  katika kuthaminisha  almasi na vito kwa ajili ya kukokotoa mrabaha wa Serikali; Kutayarisha miongozo ya bei (Price Guides)  ya almasi na madini ya  vito inayotumika kukokotoa mrabaha na  Kutoa huduma za kijemolojia (Gemmological Services) kwa wachimbaji wadogo na wa kati na Kusimamia mauzo na kufuatilia mwenendo wa masoko ya almasi na  madini ya vito.
  Kutokana na  usimamizi mzuri wa  mauzo na kufuatilia mwenendo wa masoko ya almasi na  mad  ini ya vito, ulipelekea wastani wa bei ya almasi za Tanzania katika soko la dunia kupanda hadi  dola za Marekani 286 kwa karati   ikiwa ni ongezeko la  asilimia 13, alisisitiza Kalugendo
Alisema  masoko saba ya kimataifa yalifatiishwa ili kutambua mwenendo wa bei na masoko ya madini ya vito na almasi duniani ambayo ni  Bangkok, Antwerp, Basel, London, Changsha, Las Vegas na Arusha.
Kalugendo aliongeza  kuwa  mafanikio yaliyopatikana kutokana na usimamizi mzuri wa shughuli za uthamini wa almasi na madini ya  vito  ni pamoja na  mauzo ya Tanzanite kuliingizia  Shirika la Madini la  Taifa (Kalugendo aliainisha mafanikio mengine yaliyopatikana kuwa ni pamoja na Kilo 818, gramu 269,211 na carat 40,599 za Tanzanite kuthaminiwa na kuuzwa na mgodi wa TanzaniteOne Minerals Limited (TML) wa Arusha.
Akielezea changamoto za TANSORT  Kalugendo alisema ni pamoja na kada ya  Wajemolojia kutokuwa katika muundo wa Kada za Utumishi wa Umma , kutokuwepo kwa kituo  maalum  cha kufanyia biashara ya almasi na vito nchini na kuendelea kwa vitendo vya wizi, udanganyifu, utapeli na utoroshwaji wa madini ya almasi na vito nchini.
 Kalugendo aliendelea kueleza kuwa  kumekuwepo a  ukwepaji wa kodi na tozo za Serikali miongoni mwa wazalishaji na wafanyabiashara wadogo wa almasi na vito hali inayopelekea taifa kukosa mapato yake stahiki.
Akielezea mikakati katika utatuzi wa changamoto hizo Kalugendo alisema  rasimu ya Kada ya Wajemolojia imekamilika kwa ajili  ya taratibu  zinazofuata pamoja na matayarisho kwa ajili ya  soko rasmi la kuuzia madini ya thamani kubwa hapa nchini  kuendelea kufanyiwa kazi na Wizara.
Alisema  hatua mbalimbali  zinazoendelea ni pamoja na kufanya tathmini za mapato, kutafuta uwekezaji katika jengo hilo, kutathmini namna bora ya kuendesha soko hilo na kujifunza kutoka nchi nyingine juu ya uendeshaji bora wa masoko ya jinsi hiyo.
Aidha, aliongeza kuwa TANSORT imejipanga kuendelea kutoa elimu  juu ya athari za vitendo vya udanganyifu, wizi, ukwepaji kodi, na utoroshaji wa madini ya vito.
TANSORT ni Kitengo cha Uchambuzi na Uthamini wa Madini ya Almasi na Vito cha Wizara ya Nishati na Madini ambapo uthamini unalenga ukokotoaji sahihi wa mrabaha wa Serikali kama ilivyoelekezwa na Sheria ya Madini ya Mwaka 2010, Vifungu vya 87, 88 na 89.  Kitengo hiki kilichoanzishwa mwaka 1966 kina ofisi tano  sehemu tofauti tofauti ikiwa ni pamoja na Antwerp nchini Ubeljiji,  Kanda ya Mashariki (Dar es Salaam) Kanda ya  Kati- Magharibi (Shinyanga) Kanda ya Kaskazini (Arusha) Kanda ya Kusini (Songea).

No comments:

Post a Comment