Friday, August 8, 2014

KOMBE LA KAGAME KUTIMUA VUMBI LEO, AZAM FC KUTUPA KARATA YA KWANZA NA RAYON

 
 Na Baraka Mpenja

Imechapishwa Agosti 8, 2014, saa 3:23 asubuhi

MICHUANO ya Kombe la Kagame inaanza kutimua vumbi leo hii Agost 8 hadi 24 mwaka huu mjini Kigali nchini Rwanda,  ambapo timu 14 zitawania taji linaloshikiliwa na mabingwa watetezi, Vital’O ya Burundi.
Wawakilishi wawili wa Tanzania katika michuano hiyo, KMKM ya visiwani Zanzibar na mabingwa Tanzania wa ligi kuu soka Tanzania bara, Azam fc watashuka dimbani leo katika mechi za ufunguzi.
KMKM watacheza mechi ya ufunguzi ya kundi A dhidi Altabara ya Sudan kusini katika uwanja wa Nyamirambo.
Wana Lambalamba, Azam fc waliopo kundi moja A  timu hiyo ya Zanzibar, watajitupa uwanjani jioni kuoneshana ufundi na wenyeji Rayon Sport katika dimba la taifa, Amahoro mjini Kigali.
Azam fc waliokwenda Kigali na kikosi kamili gado wanatazamiwa kutoa upinzani mkubwa wa Rayon ambao watakuwa na faida kubwa ya mashabiki.
Baada ya mechi ya Azam, usiku katika dimba hilo hilo, mchezo mmoja wa kundi B utachezwa baina ya timu ya zamani ya kocha wa Simba sc, Zdrvako Logarusic na KCCA ya Uganda.
Kesho Agosti 9 mwaka huu katika dimba la Amahoro  mechi mbili za kundi C na moja ya kundi B zitapigwa.
Mapema itaanza mechi ya mabingwa Vital’O ya Burundi dhidi ya Benadir ya Somalia ikifuatiwa na mechi ya jioni baina ya Police ya Rwanda na El Merreikh ya Sudan.
Baadaye usiku maafande wa jeshi, APR ya Rwanda watachuana na Flambeau ya Burundi.
Azam fc watashuka dimbani tena Agosti 10 mchana kuchuana na KMKM ya Zanzibar, mchezo wa kundi A.

No comments:

Post a Comment