Thursday, September 25, 2014

SERIKALI KUTATUA TATIZO LA MAKAZI KWA WATUMISHI


Fatma Salum-Maelezo

Serikali imejipanga kutatua tatizo la makazi kwa watumishi wa umma kwa kujenga nyumba Elfu 10 za gharama nafuu kote nchini.

Hayo yamesemwa jijini Dar es Salaam na Mtendaji Mkuu wa  Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) Bw.Elius Mwakalinga wakati wa ziara ya waandishi wa habari katika miradi mbalimbali inayotekelezwa na wakala huo jijini Dar es Salaam na Pwani.

 Mwakalinga alisema kuwa  mradi huo wa nyumba elfu 10 unaogharimu zaidi ya shilingi bilioni 18 unahusisha nyumba za viongozi na watumishi wa kawaida wa kada zote.

“Lengo la kujenga nyumba hizi ni kuwapatia  watumishi wa umma makazi bora jirani na maeneo yao ya kazi ili kuongeza tija katika utoaji huduma kwa wananchi. Mradi huu utawawezesha kupata nyumba za kupanga na  kununua kwa gharama nafuu”.  Alisema Mwakalinga.

 

Akifafanua zaidi  Mwakalinga alisema kuwa fedha za kutekeleza mradi huo zinatokana na ruzuku ya serikali pamoja na fedha za TBA ambapo kwa mkoa wa Dar es Salaam nyumba hizo zimeanza kujengwa kwenye maeneo ya Bunju, Mbezi Beach, Ada Estate na Masaki na pia eneo la Chalinze mkoani Pwani.

 

Aidha Kaimu Mkurugenzi wa Ushauri kutoka TBA Bw. Edwin Nnunduma alisema kuwa ujenzi wa nyumba hizo unatumia teknolojia ya kisasa inayopunguza gharama na muda wa kukamilika.

 

Pia Nnunduma alisema mpaka sasa ujenzi unaendelea vizuri kwenye mikoa mbalimbali nchini ikiwemo mikoa mipya ya Katavi, Geita, Simiyu na Njombe.

 

Naye Meneja wa Kikosi cha Ujenzi cha TBA Mhandisi Wilfred Dungamu alieleza kuwa kwa sasa wakala huo unatumia kikosi cha wahandisi wa ndani kilichoanzishwa mwaka 2012 na mpango huo umesaidia kupunguza gharama kubwa zilizokuwa zikitumika kuwalipa wahandisi kutoka makampuni binafsi.

No comments:

Post a Comment