Friday, September 5, 2014

YANGA SC YA MARCIO MAXIMO KUIVAA BIG BULLETS JUMAPILI, KIINGILIO KWA 'WASAKA TONGE' BUKU TANO TU!


Kocha Mkuu wa Young Africans Marcio Maximo (kushoto) akiongea na waandishi wa habari juu ya mchezo wa kirafiki dhidi ya Big Bullets kutoka Malawi siku ya jumapili, kulia ni Afisa Habari wa timu hiyo Bw Baraka Kizuguto

Na Mwandishi Wetu, Dar es salaam

TIMU ya Young Africans itashuka dimba la Uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam siku ya jumapili kucheza mchezo wake wa mwisho wa kirafiki wa kimataifa dhidi ya timu ya Big Bullets FC (zamani Bata Bullets) inayoshiriki Ligi Kuu ya TNM nchini Malawi.
Young Africans ambayo imeshacheza michezo minne mpaka sasa ya kirafiki ukiwemo mmoja wa kimataifa katikati ya wiki hii dhidi ya timu ya Thika United kutoka nchini Kenya imeshinda michezo yote.
Akiongea na waandishi wa habari leo katika mkutano na waandishi wa habari, kocha mkuu wa Young Africans mbrazil Marcio Maximo amesema mchezo huo wa siku ya jumapili utakua ni kipimo kizuri kwa vijana wake kabla ya kuanza kwa Ligi Kuu ya Vodacom wiki mbili zijazo.
"Mchezo uliopita tuliocheza dhidi ya Thika United ulikua ni mchezo mzuri, tumepata nafasi ya kuyaona mapungufu yetu na kama mnavyofaham wenzetu wako katika Ligi inayondelea hivyo walicheza kitimu zaidi kuliko sisi na hata Big Bullets FC pia namini kitakua ni kipimo kizuri kwetu " alisema Maximo". 
Kuhusu timu ilivyocheza Maximo amesema hapendi kumzungumzia mchezaji mmoja mmoja, na masula ya uchezaji hapendi kuyaongea kwa jamii, hiyvo yeye kama kocha alishaongea na wachezaji na kuwaelezea mapungufu yaliyojitokea na kipi wanapaswa kukifanya katika michezo inayofuata.
Aidha Maximo aliongeza kuwa yeye kwa sasa hana kikosi cha kwanza, hana mchezaji mwenye uhakika wa namba, kilichopo kwake ni kundi la wachezaji ambao wote wana nafasi ya kucheza kulingana na mahitaji ya mchezo wenyewe.
Afisa Habari wa Young Africans Bw Baraka Kizuguto amesema taratibu zote za mchezo zimekamilika na timu ya Big Bullets FC kutoka nchini Malawi inatarajiwa kuwasili kesho jijini Dar es salaam na kufanya mazoezi jioni katika Uwanja wa Karume eneo la Ilala.
"Mchezo wa jumapili tunatarajia utakua ni mchezo mzuri, ukizingatia timu ya Big Bullets FC inashika nafasi ya pili kwenye msimamo wa Ligi Kuu nchini Malawi iiliyofikia mzunguko wa 17 kwa tofauti ya pointi moja na vinara, na kocha Maximo alipendekeza tupate timu tofauti kutoka ukanda wa Kusini mwa Afrika baada ya kuwa tayari tumeshacheza na timu ya Ukanda wa Afrika Mashariki" alisema Kizuguto. 
Siku ya jumapili mechi inatarijiwa kuanza majira ya saa 10 kwa saa za Afrika Mashariki na viingilio vya mchezo ni kama ifuatavyo:
VIP A Tshs 30,000/=
VIP B & C Tshs 20,000/=
Orange Tshs 10,000/=
Blue & Green Tshs 5,000/= 

No comments:

Post a Comment